Wednesday, November 18, 2015

WANGA BADO MAPEMA KUANZA KUNIHUKUMU

Posted By: kj - 6:14 PM

Share

& Comment

NYOTA wa timu ya Azam FC, Allan Wanga, amesema ni mapema mno kwa mashabiki wa timu hiyo kuanza kuhoji uwezo wake, huku akiwaambia kuwa muda si mrefu wataanza kuona cheche zake.

Wanga alitua Azam FC Julai mwaka huu baada ya kugoma kuongeza mkataba katika timu yake ya awali ya El Merreikh ya Sudan.

Nyota huyo kutoka Kenya aliuambia mtandao wa azamfc.co.tz hivi karibuni kuwa, jambo kubwa lililomfanya asiwe kwenye kasi yake ni matatizo ya kufiwa na mama yake mzazi, aliyopata kabla ya kuanza kwa msimu mpya.

“Kwa sasa ni mapema sana kuanza kuhoji kiwango changu, nilikosa sehemu kubwa cha maandalizi ya msimu na hata mechi za kirafiki sikucheza, wakati nashughulikia msiba wa mama yangu, hivyo hivi sasa najaribu kujiweka fiti na wenzangu, mashabiki watarajie makubwa kutoka kwangu.

“Hivi sasa mimi bado ni mgeni Azam FC, najaribu kuingia kwenye mfumo mpya wa timu, ambao ni tofauti na kule nilipokua, naamini nitaanza kufanya vizuri zaidi katika siku za usoni,” alisema.

Wanga aliyewahi kukipiga nchini Vietnam katika timu ya Hoang Anh Gia Lai, Petro Atletico ya Angola, FC Baku ya Azerbaijan, Tusker na AFC Leopards za Kenya, aliongeza kuwa Ligi Kuu ya Sudan ina ushindani mkubwa sana tafauti na Tanzania hata kwa timu zinazoshika nafasi za chini.

Mpaka sasa akiwa ameichezea Azam FC takribani mechi nne, amefanikiwa kufunga bao moja, alilotupia wakati timu hiyo ilipoilaza Stand United mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Kambarage, Shinyanga.

Azam FC inayodhaminiwa na Benki ya NMB, kwa sasa ipo kileleni kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 25 baada ya kushinda mechi nane na kutoa sare mchezo mmoja dhidi ya Yanga, ambayo inafuatia katika nafasi ya pili ikiwa nazo 23.

0 Maoni:

Post a Comment

Copyright © CHAMA LANGU NI AZAM FC™ is a registered trademark.

Designed by Templateism. Hosted on Blogger Platform.