Monday, November 7, 2011

Mwadini, Kaseja wampagawisha Poulsein

Posted By: kj - 9:47 AM

Share

& Comment


WALINDA mlango Juma Kaseja (Simba) na Mwadini Ally (Azam FC), wamemweka katika wakati mgumu kocha mkuu wa timu ya Taifa 'Taifa Stars', Jan Poulsen kuamua kuwa atamwanzisha nani kwenye mchezo dhidi ya Chad wa kutafuta nafasi ya kutinga hatua ya makundi ya kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil.

Mchezo huo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, umepangwa kufanyika Novemba 11 nchini Chad na Taifa Stars ambayo hivi sasa ipo kambini ikijiandaa mechi hiyo inatarajia kuondoka nchini kesho ikiwa na kikosi cha wachezaji 20.

Akizungumza na Mwananchi jana, Poulsen alisema kuwa tangu timu hiyo ilipoingia kambini amekuwa akivutiwa zaidi na uwezo wa makipa hao ambao pia walifanya vizuri katika Ligi Kuu mzunguko wa kwanza.

Alisema makipa hao wamekuwa wakifanya vizuri zaidi mazoezini jambo ambalo linamfanya awe na wakati mgumu kuamua kuwa ni nani atakayempanga kuanza katika kikosi cha kwanza cha timu yake kitakachopambana na Chad Ijumaa ya Novemba 11 kabla ya kurudiana Novemba 15 jijini Dar es Salaam.

"Tunaendelea vizuri na maandalizi yetu vijana wote wapo katika hali nzuri ambayo inatupa matumaini makubwa ya kufanya vema katika mechi yetu dhidi ya Chad japokuwa tunaweza kumkosa Nadir Haroub (Canavaro) ambaye anasumbuliwa na majeruhi.

"Ukiachana huyo wachezaji wengine wote wapo vizuri kabisa na wamekuwa wakifanya vema kwa kila wanachopaswa kufanya na kuonyesha ushindani wa hali ya juu, hata hivyo nafasi ya makipa kwa hakika naweza kusema ndiyo wanaongoza.

"Kaseja na Mwadini wamekuwa wakionyesha kiwango kizuri ambacho kwa hakika kitanipa wakati mgumu kuamua nani ataanza katika kikosi cha kwanza hivyo Novemba 11," alisema Poulsen.



Mwananchi

0 Maoni:

Post a Comment

Copyright © CHAMA LANGU NI AZAM FC™ is a registered trademark.

Designed by Templateism. Hosted on Blogger Platform.