Tuesday, December 3, 2013

OMONG KUANZA NA MAMBO MATATU

Posted By: Unknown - 6:26 AM

Share

& Comment

JOSEPH Omong ambaye ni raia wa Cameroon, ndiye kocha mpya wa Azam FC. Ameshasaini mkataba wa miaka miwili wa kuifundisha timu hiyo ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

Omong alitua Dar es Salaam juzi Jumamosi akiongozana na mtoto wake wa kwanza, Erick, ambaye ndiye meneja wake na leo Jumatatu ndiyo anaanza kazi.

Kocha huyo amesisitiza kuwa amekuja Tanzania kufanya mambo matatu ambayo ni lazima ayakamilishe ndani ya mwaka mmoja; la kwanza ni kuipa Azam ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, pili ni kuandika historia mpya kwa kufanya vizuri Kombe la Shirikisho na tatu ni kuwaendeleza vijana wa Azam Academy.

Malengo ya kocha huyo yanawapa matumaini mabosi wa Azam ambao kupitia Makamu Mwenyekiti wao, Said Mohamed, wamempa hadhi ya kuwa ‘Bingwa wa makocha’.

Hiyo ni kutokana na historia yake ya nyuma alipokuwa na A.C Leopards ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Brazaville ambayo ilikuwa haijapata upingwa wa ligi kwa miaka 30.

Alitumia utaalamu wake katika kuipa timu hiyo mafanikio kwani walitwaa ubingwa wa Ligi Kuu Congo Brazaville kwa misimu miwili mfululizo wa 2012 na 2013.

Kubwa zaidi ni pale A.C Leopards ilipotwaa ubingwa wa Kombe la Shirikisho Afrika mwaka jana, na mwaka huu Leopards ilitolewa kwenye hatua ya makundi kwa michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Anakuwa kocha wa tano wa kigeni kuifundisha Azam baada ya Wabrazili, Neider dos Santos na Itamar Amorin. Wageni wengine waliopita hapo ni Stewart Hall (Mwingereza) na Boris Bunjak (Mserbia).

Mwanaspoti ilipofanya mazungumzo na kocha huyo kupitia ukalimani wa mwanaye, Erick, anayeweza kuzungumza Kiingereza kwa ufasaha, kocha huyo anayezungumza zaidi Kifaransa anasema: “Mtazamo  wangu uko mazoezini, huko ndiko nitaangalia namna gani tutafanikiwa na siyo jambo lingine, nahitaji kukaa na wachezaji ili kuwafahamu vizuri na jinsi watakavyokamilisha malengo yangu.

“Nimekaa na uongozi kwa muda, tukazungumza na kukubaliana, najua malengo ya timu ambayo ndiyo nitayafanyia kazi. Naahidi kuwapa ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu, kufanya vizuri na kuandika historia katika michuano ya Kombe la Shirikisho pamoja na kuendeleza Academy ya klabu.”

Kuhusiana na kuikuta ligi katikati huku yeye akiwa hana uzoefu wa soka la Tanzania, alisema: “Nitafanikisha malengo yangu kwani sioni sababu ya kushindwa.”

Omong anasema, anafahamu Azam ni timu kubwa na aliifahamu iliposhiriki Kombe la Shirikisho Afrika kabla ya kutolewa na Wamorroco (AS FAR RABAT). Anasema anafahamu timu hiyo iliitoa Al Nasir Juba ya Sudan Kusini kwa jumla ya mabao 8-1 na Barack Young Controllers II ya Liberia kwa jumla ya mabao 2-1.


Simba na Yanga/Lugha
Klabu za Simba na Yanga ndiyo kongwe na maarufu nchini, lakini Omong anasema hazifahamu kabisa klabu hizo.

“Sizijui Simba wala Yanga, lakini mimi ni kocha mwenye filosofi yangu, sioni kama itakuwa shida kwangu,”anafafanua.

 Akizungumzia lugha anasema: “Sijui Kiswahili, najua Kiingereza kidogo, Kifaransa ndiyo lugha yangu. Lakini sidhani kama kutakuwa na tatizo katika kuwasiliana na wachezaji kwa sababu mpira ni ufundi na unazungumza lugha moja.”


Wasifu wake
Omong ana umri wa miaka 63. Wakati uchezaji wake, alicheza nafasi za beki wa kati na kiungo mkabaji. Ana watoto wanne wakiwamo wawili wanawake, Erick ndiye wa kwanza.

Ni mchezaji wa zamani wa Dragon Yaounde ya Cameroon. Alijifunza ualimu wa michezo na elimu ya viungo katika Chuo cha Higher Institute of Youth and Sports kilichopo Yaounde, Cameroon.

Mwaka 1987 alipata Stashahada ya Ukocha wa Soka na leseni B ya ukocha kwa viwango vya Shirikisho la Soka la Ulaya (Uefa), alipata baada ya mafunzo yaliyofanyika Ujerumani.

Akiwa kwao Cameroon, Omong alizifundisha klabu za Fovu of Baham na Ainglwe of Menoua ambayo ilifuzu fainali za Kombe la Cameroon.

Mwaka 2001 alikuwa Kocha Msaidizi wa timu ya Taifa ya Cameroon ‘Indomitable Lions’ chini ya Mjerumani, Winfried Schafer na mwaka 2010 aliinoa timu ya Taifa ya Cameroon kwa wachezaji wa ndani kabla ya kutimkia Congo.

Omong sasa ndiye amebeba roho ya Azam. Ni wazi timu hiyo imepata kocha mwingine bora mwenye uzoefu wa kufanya kazi na wachezaji maarufu duniani kama vile Samuel Eto’o na Alex Song.

Lakini uongozi na wamiliki wa Azam wanapaswa kujua kwamba kocha huyo atahitaji muda ili kuleta mafanikio Chamazi, hivyo wanapaswa kuwa tayari kuwa na subira.

Vinginevyo itaendeleza wimbi lake la kuwabadilisha makocha. Katika msimu wake wa kwanza ligi kuu, Azam ikiwa bado inaundwa na wachezaji wengi waliopandishwa timu, ilimfukuza Santos baada ya kufungwa na Simba SC.

Itamar aliondoka kwa sababu ya kuzidiwa nguvu na wachezaji wasio na nidhamu mbele ya uongozi wakati Hall mara ya kwanza aliondolewa tu katika mazingira ambayo hayakueleweka, walimchoka tu na wakamwajiri Bunjak.

Mserbia huyo naye, pamoja na kuiongoza vizuri timu ikiwa kwenye mbio za ubingwa hadi mwishoni mwa mzunguko wa kwanza, baada ya kufungwa na Simba naye akafukuzwa. Akarudi Stewart na akafanikiwa kuzifunga Simba na Yanga katika ligi msimu huu, lakini haikutosha baada ya mzunguko wa kwanza, akaambiwa aondoke. Sasa timu iko mikononi mwa Omong, tusubiri kuona atakachofanya.



CHANZO: MWANASPOTI

0 Maoni:

Post a Comment

Copyright © CHAMA LANGU NI AZAM FC™ is a registered trademark.

Designed by Templateism. Hosted on Blogger Platform.