MATUMIZI
ya tiketi za kisasa za kieletroniki katika viwanja vitakavyotumika kwa
mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara, yataanza kwa majaribio katika Uwanja wa
Azam Complex kuanzia mwakani.
Awali, mfumo huo unaolenga
kudhibiti mapato na kuondoa usumbufu kwa mashabiki kupanga foleni siku
za mechi, ulipangwa kuanza mwaka jana na baadaye kuahirishwa na kutakiwa
kuanza Januari, lakini imeshindikana kutokana na kudaiwa kukawia
kuwasili kwa mashine zitakazofungwa katika viwanja husika.
Akijibu
maswali ya waandishi wa habari Dar es Salaam wiki hii, Rais wa
Shirikisho la Soka Tanzania(TFF), Jamal Malinzi alisema tayari mashine
zimeshafungwa karibu viwanja vyote isipokuwa viwili kile cha Ali Hassan
Mwinyi mkoani Tabora na cha Kaitaba mjini Bukoba mkoani Kagera.
“Kudhibiti
wizi wa tiketi ni changamoto kubwa, lakini niseme kwamba suala hilo
tutalifanyia kazi, lakini kwa kuanza majaribio kwenye Uwanja wa Azam
Complex, ndipo tutaendelea na sehemu nyingine,” alisema Malinzi
aliyeingia madarakani Oktoba 27, mwaka huu.
Alisema lengo la
kuanza na uwanja mmoja ni kutaka kuona kwanza utendaji wake
utakavyokuwa, kama utasaidia ndipo viwanja vingine vitaruhusiwa
kuendelea na mpango huo.
Mpango wa kutumia mfumo huo ni matokeo
ya juhudi mbalimbali za TFF kutafuta njia bora itakayodhibiti mapato ya
viwanjani na kuondoa usumbufu kwa wapenzi kupanga foleni siku ya mechi
au siku chache kabla.
Kufanikiwa kwa mfumo huo ni baada ya Benki
ya CRDB, kushinda zabuni ya kazi hiyo baada ya mchakato ulioshirikisha
kampuni mbalimbali zilizotuma maombi yao.
CHANZO: HABARI LEO
Saturday, December 7, 2013
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Maoni:
Post a Comment