Friday, March 4, 2016

NI AZAM NA TANZANUA PRISONS ROBO FAINALI

Posted By: dada - 4:50 PM

Share

& Comment


KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, imepangiwa kucheza na Tanzania Prisons ya mkoani Mbeya kwenye mchezo wa hatua ya robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup).

Azam FC inayodhaminiwa na Benki ya NMB imefika hatua hiyo baada ya kuitoa Panone kwa kuipa kichapo cha mabao 2-1, yaliyofungwa na Pascal Wawa na Allan Wanga, huku Tanzania Prisons nayo ikipata ushindi kama huo ilipowatoa wapinzani wao Mbeya City katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Kwa mara ya kwanza tokea kuanza kwa michuano hii msimu huu, waandaaji ambao ni Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wamepanga Azam FC kucheza nyumbani dhidi ya maafande hao, mchezo utakaofanyika Machi 31 mwaka huu (Alhamisi) katika Uwanja wa Azam Complex.

Hiyo inatokana na TFF kuipangia Azam FC kucheza mechi mbili za awali ugenini kwenye viwanja visivyoridhisha, ya kwanza ikiwa dhidi ya African Lyon waliyoshinda mabao 4-0 ndani ya Uwanja wa Karume na nyingine iliyopita waliyokipiga na Panone katika Uwanja wa Ushirika mjini Moshi.

Kwa timu zote zilizoingia hatua ya robo fainali, ni Azam FC pekee ambayo imecheza mechi zake zote zilizopita ugenini.

Azam FC imejiwekea malengo ya kutwaa taji la michuano hiyo, ambayo ndio itatoa bingwa atakayeiwakilisha Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAF CC) mwakani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na TFF, wamedai kuwa droo ijayo ya michuano hiyo wataifanya ikiwa moja kwa moja kwenye luninga (live), itakayofanyika Aprili 7 mwaka huu.

Mechi nyingine za robo fainali;
* Geita Gold vs Mwadui (Machi 26, 2016, Uwanja wa Kirumba, Mwanza)
* Yanga vs Ndanda (Machi 31, 2016, Uwanja wa Taifa, DSM)
* Simba vs Coastal Union (Aprili 6, 2016, Uwanja wa Taifa, DSM)

0 Maoni:

Post a Comment

Copyright © CHAMA LANGU NI AZAM FC™ is a registered trademark.

Designed by Templateism. Hosted on Blogger Platform.